Habari za Hivi Punde

6/recent/ticker-posts

PAMBA YAPATA NGUVU MPYA: CHUPA MILIONI 8 ZA VIUATILIFU KUPAMBANA NA WADUDU WAHARIBIFU


Katibu wa chama cha wanunuzi wa pamba TCA , Boaz Ogolla akizungumza na waandishi wa habari za Pamba.

Na Marykitoto 

Sekta ya pamba nchini imepata nguvu mpya baada ya Chama cha Wanunuzi wa Pamba Tanzania (TCA) kupokea chupa milioni 8 za dawa za kuua wadudu waharibifu wa zao hilo, zilizotolewa na Serikali kupitia Bodi ya Pamba Tanzania (TCB).

Hadi sasa, chupa milioni 6 tayari zimesambazwa kwa wakulima nchini, zikiwa na lengo la kudhibiti wadudu wanaofyonza na kutafuna vitumba vya pamba—wanaosababisha hasara kubwa ya mavuno.


Dawa za Pamba zinazotolewa na Bodi ya Pamba kwa ajili ya kudhibiti wadudu wanaoshambulia zao la pamba.

Akizungumza na waandishi wa habari, Katibu wa TCA, Boaz Ogolla amesema hiki ni kipindi muhimu kwa wakulima kuchukua hatua dhidi ya wadudu wanaoharibu mazao yao.

Serikali pia imekuja na mkakati maalum wa kutumia teknolojia za kisasa kama ndege nyuki (drones), maboza na matrekta ili kuongeza ufanisi katika kudhibiti wadudu mashambani.

Kwa upande wake, TCA imejipanga kuhakikisha dawa zinawafikia wakulima hadi vijijini, sambamba na kutoa elimu sahihi ya matumizi ya viuatilifu kupitia vijana wa BBT.

Kwa wakulima wa pamba hai (organic), tayari wamepokea dawa asilia (biopesticides) na zoezi la kudhibiti wadudu linaendelea mashambani.

Aidha, mfumo wa BBT umewezesha kila mnunuzi wa pamba kupewa eneo la kuwekeza, hatua inayolenga kuongeza uzalishaji na kusimamia wakulima kwa karibu zaidi.

Ogolla amesema Tanzania inaendelea kuonyesha mafanikio katika uzalishaji wa pamba mwaka hadi mwaka, huku akisisitiza umuhimu wa usimamizi wa Serikali katika sekta hiyo.

Post a Comment

0 Comments