Na mwandishi wetu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewasilisha ujumbe maalum kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), António Guterres, akisisitiza dhamira ya Tanzania kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kudumisha amani na kuhimiza maendeleo endelevu duniani.
Ujumbe huo uliwasilishwa Juni 16, 2026 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, kwa niaba ya Rais Samia wakati wa mazungumzo yake na Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa.
Katika mazungumzo hayo, pande zote mbili zilijadili masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa pamoja na mchango wa Tanzania katika kuendeleza amani, utulivu na maendeleo ya kimataifa.
Baada ya mazungumzo hayo, Balozi Kombo alimkabidhi António Guterres zawadi ya kitabu kinachoelezea maisha na mchango wa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Rais wa Kwanza wa Tanzania.
Hatua hiyo ililenga kutambua na kuthamini kuvutiwa kwa muda mrefu kwa Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa na maono, uongozi na mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhimiza amani, maendeleo na ushirikiano wa kimataifa.
Tanzania imeendelea kudumisha uhusiano mzuri na Umoja wa Mataifa kupitia ushiriki wake katika masuala ya amani, maendeleo na diplomasia ya kimataifa, huku Serikali ya Rais Samia ikiendelea kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia.
Mwisho.
0 Comments