Habari za Hivi Punde

6/recent/ticker-posts

DARAJA LA MILIONI 254.4 LAWA MKOMBOZI KWA WANANCHI WA BUSEGA.

 



Na mwandishi wetu 

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha, tarehe 12 Juni 2016 alikagua ujenzi wa Daraja la Mawe lililopo katika Barabara ya Ngasamo–Gininiga, Wilaya ya Busega, na kuwataka wananchi kuhakikisha wanalinda miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.


Mhe. Macha alifanya ukaguzi huo akiwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo yenye lengo la kufuatilia na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa kwa manufaa ya wananchi.



Daraja hilo linaunganisha vijiji vya Gininiga, Nyangoko na Ngasamo, na limejengwa kwa gharama ya shilingi milioni 254.4. Fedha za ujenzi huo zimetolewa na wadau wa maendeleo kupitia Benki ya Dunia, huku usimamizi wa mradi ukifanywa na TARURA.


Akizungumza na wananchi waliojitokeza katika eneo la mradi huo, Mhe. Macha aliwasisitiza kulinda miundombinu ya daraja pamoja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika kuhusu watu wanaojihusisha na vitendo vya uharibifu wa miundombinu ya barabara, ikiwemo ukataji wa vyuma kwenye kingo za daraja.


“Ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha miundombinu hii inalindwa. Wale wanaoharibu mali za umma wanapaswa kufichuliwa ili hatua stahiki zichukuliwe,” alisema Mhe. Macha.



Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wananchi kuacha tabia ya kuchimba mchanga, mawe na madini ya ujenzi karibu na hifadhi za madaraja na barabara, akieleza kuwa vitendo hivyo vinachangia kwa kiwango kikubwa uharibifu wa miundombinu na kuhatarisha usalama wa watumiaji wa barabara.


Kwa mujibu wa wananchi wa eneo hilo, Daraja la Mawe la Ngasamo limekuwa mkombozi mkubwa kwa wakazi wa Kata za Ngasamo na Malili kwa kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa, hali inayochochea shughuli za kiuchumi na maendeleo ya kijamii katika maeneo hayo.


Kukamilika kwa daraja hilo kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuboresha mtandao wa usafiri na usafirishaji Wilaya ya Busega, huku likitarajiwa kuongeza fursa za biashara, upatikanaji wa huduma za kijamii na kukuza uchumi wa wananchi kwa ujumla.

Mwisho.





Post a Comment

0 Comments